HATUA YA TISA BORA YA LIGI DARAJA LA TATU JIJINI MWANZA KUANZA MWISHONI MWA MWEZI HUU.

Hatua ya tisa bora katika ligi daraja la tatu mkoani Mwanza inatarajiwa kuanza kutimua vumbi kuanzia Februari 26 mwaka huu kwenye  uwanja wa kisasa wa  Nyamagana Jijini Mwanza.


Katibu wa chama cha mpira wa miguu mkoa wa Mwanza (MZFA), Leonard Malongo aliyasema hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake.

Alisema kamati ya mashindano inatangaza rasmi timu zilizofuzu hatua ya tisa bora (fainali) kutoka  vituo viwili vya Nyehunge na Ngudu huku Nyamagana wakisubiria kukamilisha michezo ya hatua ya kwanza inayotegemewa kumalizika  Februari 18 mwaka huu.

Malongo alizitaja timu zilizofuzu kwenye hatua hiyo katika kituo cha Nyehunge kuwa ni Singa FC yenye pointi 12, Mwanza Ndovu pointi 7, Iseni FC pointi sita huku kituo cha Ngudu kikiwa na timu ya Igoma Heroes yenye pointi 15, Black Mamba pointi 13 na Vijana FC pointi 11.

Alisema kamati inaagiza viongozi wa timu ziliofuzu hatua ya fainali ambao ni Makatibu na timu meneja kuhudhuria kikao cha maandalizi Februari 19 mwaka huu katika uwanja wa CCM Kirumba majira ya saa 04:00 asubuhi kwa ajili ya kujadiliana, kukumbushana kanuni  pamoja na kutoa utaratibu wa kuboresha  ikosi vyao kwani  chama kimetoa siku saba za kuongeza na kusajili wachezaji watano ili kuweza kujiandaa na fainali hiyo.

Hata hivyo alisema wamezishusha daraja timu za Kisesa Star, Igogo FC, Mwanza City na TSC Academy kutokana na  kushindwa kufika viwanjani  pamoja na kujiondoa kwenye mashindano wakati ligi imekwisha anza.

Sambamba na hayo alisema wamemfungia mchezaji  John Evarist kujihusisha na mpira wa miguu  kwa miezi  kumi na mbili baada ya kudanganya jina  ili acheze vilabu viwili  kwa wakati mmoja ambavyo ni Singa FC ambapo alitumia jina la John Evarist huku timu ya Buselesele FC akitumia John Otaka hivyo kwa mujibu wa kanuni  namba 50 (1) imemkataza mchezaji yoyote  atakaye badili jina lake halisi  kwa madhumuni ya kudanganya  ili asajiliwe na kwamba akigundulika atafungiwa kucheza mpira ndani na nje ya nchi kwa kipindi  kisichopungua miezi kumi na mbili kuanzia siku atakayo bainika.

Aidha alisema timu ya Singa FC imepigwa faini ya Tsh. 800,000 baada ya kumchezesha mchezaji John Evarist michezo minne na fedha hizo zinatakiwa  kulipwa kabla ya kushiriki hatua inayofuata ya tisa bora ikiwa hiyo ni kwa mujibu wa kanuni namba 50 (2) inayosema  “Klabu iliyo mchezesha  mchezaji  aliyebadilisha jina  kwa nia ya kudanganya italipa faini ya Tsh. 200,000 kwa kila mchezo ambao  mchezaji huyo alicheza lakini matokeo hayata badilika”.

Pia aliongeza kuwa kamati imemfungia Katibu wa Singa FC Eladius Atanas kujihusisha na masuala ya mpira wa miguu kwa muda wa miezi sita kuanzia Februari 13 mwaka huu kwa kutoa taarifa za uongo kuhusu mchezaji John Evarist kwa mujibu wa kanuni namba 50(8) inayosema “ Kiongozi yeyote wa chama cha mpira wa miguu au kilabu atakayetoa taarifa za uongo na kupotosha chama cha mpira wa miguu cha mkoa husika katika maamuzi yake kuhusiana na usajili atakabiliwa na adhabu ya kufungiwa kwa kipindi kisichopungua miezi sita.

No comments