SINGIDA UNITED INAKWENDA MBELE NA KURUDI NYUMA.
ILIKUJA kama timu tishio
iliyozitisha timu nyingi. Timu inayofundishwa na Hans Van Pluijm, yenye
wachezaji wa kariba ya Shaffiq Batambuze, Danny Usengimana, ilimtisha kila
mmoja.
Singida United ilitisha kimtazamo,
ilitisha kwa mikataba minono iliyosaini na kufanya jezi zao zichafuke kwa
matangazo mbalimbali bado ikaja kututisha ndani ya uwanja kwa kupiga soka la
Kiholanzi 'Total football '.
Mashabiki Simba, Yanga walianza
kuitazama Singida United kama mshindani wao mwingine kando ya Azam Fc ambaye
amekaa katikati yao. Waliihofia sana timu hii.
Wakati yote yanafanyika, huwezi
kuamini ukiambiwa timu hii ndiyo kwanza ilikuwa imepanda daraja la ligi kuu
kama ilivyokuwa kwa Njombe Mji na rafiki zangu wa Lipuli Fc.
Muonekano wa Singida United
uliwafanya wasionekane kama timu iliyopanda daraja ambayo mafanikio yake
makubwa yanakuwa kubakisha timu isishuke ndani ya msimu mmoja.
Maisha yao yakawa mazuri. Wachezaji
wao wakaishi pepo ndogo ndani ya Singida yenye vijiji vizuri na tulivu kama
Itotolo.
Hali yao ikawafanya wasiwekwe katika
daraja la Lipuli Fc wala Njombe Mji, haraka kabisa nao wakawa timu inayotajwa
kushinda taji. Maisha yameenda kasi sana upande wao.
Wakaja Ligi Kuu Bara na kila aina ya
mbwembwe iliyokolezwa na hamasa ya Singida kwanza. Kashida zote hizi wakaenda
katika mchezo wao wa kwanza wa ligi na wakapoteza dhidi ya Mwadui FC pale
Mwadui Complex.
Matokeo hayo yaliwashangaza watu.
Kila mmoja alishangaa, inawezekana hata Singida United wenyewe waliyashangaa.
Aliyesema mpira una matokeo ya kikatili, hakuwa mbali na ukweli.
Ni kweli mpira una matokeo ya
kikatili. Yote haya yalionekana si kawaida kutokana na uwekezaji
uliofanywa ndani ya Singida United. Unapokuwa na Pluijm kisha ukawa na
Batambuze, wewe unakuwa hujaja ligi kuu kutalii kama zinavyotalii timu nyingi
ambazo zinaingilia mlango wa mbele kisha zinatokea mlango wa nyuma.
Wakati ligi ikiwa inakwenda
ukingoni, pole pole kabisa kwa mwendo wa madaha Singida United wameamua
kujitenga na vigogo. Ni kama maji yanavyojitenga na mafuta katika pipa
kubwa.
Timu yao inaanza kupungua makali.
Haitishi tena. Inawezekana wachezaji wamejisahau baada ya kutumia magari mazuri
na kulipwa mishahara minono. Inawezekana hili!
Mwishoni mwa wiki wametoka kufungwa
na Stand United tena katika dimba lao la Namfua. Si dhambi wao kufungiwa
nyumbani, lakini walikuja na mlengo huu wa kupoteza mechi na timu dhaifu kama
Stand United?
Huenda mipango yao mizuri tukaiona
msimu ujao, lakini uwekezaji waliofanya msimu huu wanapaswa kumaliza ligi hata
nafasi ya pili. Lakini bado siioni nafasi hii jinsi watakavyoipata.
Inaonekana ni mafanikio makubwa ya
wao kusalia kwenye ligi msimu huu ili ujao tuwaone tena, lakini tuambiane
ukweli kuwa Singida United hawakuwa na timu ya kubaki katika ligi kisha
wakapiga nderemo na vifijo, walikuwa na timu ya kubeba taji, si
vinginenyo.
Muda huu ambao Yanga, Azam Fc
zinajikongoja na mpinzani aliyekamilika akionekana kuwa Simba pekee, Singida
United wanashindwaje kufanya vyema mfululizo zaidi wana kazi ya kwenda mbele na
kurudi nyuma?

Post a Comment