INFANTINO,AHMAD WAMEINGIA NCHINI NA KUKUTANA NA PINGAMIZI LA FDL , NANI APANDE VPL




RAIS wa FIFA Gianni Infantino yuko nchini. Rais wa CAF Ahmad Ahmad nae yuko nchini. Kamera za ulimwengu wa soka zinaimurika Tanzania katika lenzi mbonyeo na mbinuko. 
Infantino, Ahmad wameingia nchini asubuhi ya leo wakilakiwa vizuri na wenyeji wao Waziri wa Habari, Tamaduni Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe, Mwenyekiti wa BMT Leodegar Tenga na Rais wa TFF, Wallace Karia. Ni ujumbe mzito uliowapokea marais hao wa FIFA na CAF. 

Marais hao wamekuja Tanzania muda ambao raia wake wanataka kuona soka la nchi likifika nchi ya ahadi.

Harakati za kufika nchi ya ahadi hazijaanza juzi, jana wala leo, zilianza siku nyingi tu, lakini zilikosa mwongozo wenye mtazamo chanya. 

Ni kama tumesimama sehemu baada ya mafanikio yetu ya mwaka 1980 pale Lagos tulipofuzu kucheza Mataifa Afrika kwa mara ya kwanza na ya mwisho. Tangu hapo tumeweka kituo kwa kusimama, hatujafuzu tena mpaka leo. 

Nini shida? Wapi tulipokwama? Nani hawajibiki? Maswali yote hayo yanakuja na majibu ya kitu kimoja kinachoitwa Serikali.

Serikali ndiyo wenye majibu ya anguko la soka letu na rafiki zangu wa TFF wao wanabeba sehemu ndogo ya lawama za soka la nchi kusimama.

Lawama za TFF ni kama hivi, Daraja la kwanza (FDL ) imeisha wenyewe hawajazithibitisha timu zilizopanda, badala yake wanasubiri kupitia pingamizi. Kuna timu zimekatiwa rufaa. 

Matatizo ya TFF ndiyo haya. Hivi bado tunaishi dunia ya kukata rufaa kwa maana ya kupinga matokeo ya uwanjani? 

Ina maana timu iliyoshinda uwanjani inaweza isipate nafasi ya kucheza Ligi Kuu Bara na timu itakayoshinda mezani ndiyo ipate nafasi hiyo? Kila leo tunapiga hatua za kurudi nyuma, sio mbele.

Muda huu ambao Infantino, Ahmad wako nchini timu zilizopanda daraja zilipaswa kushangilia, kujiandaa na ushiriki wao wa ligi msimu ujao, lakini badala yake timu hizo zimemaliza ligi uwanjani sasa zimehamia ligi ya mezani. Jamani wapi tunaupeleka huu mpira? 

Kinachoonekana hapa kwa yaliyotokea miaka miwili iliyopita yanaweza kutokea na mwaka huu. Kuna kula dalili hiyo. Miaka miwili iliyopita tulishuhudia Mbao FC ikipandishwa daraja, huku Geita na timu nyingine zikishushwa. Hili linaweza kutokea na mwaka huu. Dalili ziko wazi. 

Mpaka tumefikia hatua ya kujiwa na watu wazito kama Ahmad, Infantino, tunapaswa kubadilika jinsi ya uendeshaji soka. Kama wageni hao wakihadithiwa stori hii wanaweza kutupuuza ghafla. Kwanini tupuuzwe katika jambo la kipuuzi? 

Tuikatae aibu hii. Tena tuikatae na kuipinga kwa nguvu kubwa kama klabu za ulaya wanavyopinga dhambi ya ubaguzi wa rangi kwa kiasi kikubwa. 

Infantino, Ahmad karibuni, lakini haya ndiyo maisha yetu, ila rai yetu mkirudi makwenu msiende kuwaambia haya.


No comments