YANGA YAREJESHWA TENA UWANJA WA NAMFUA KWENYE ASFC

Mabingwa wa ligi kuu soka Tanzania Bara klabu ya Yanga imepangiwa kucheza na Singida United kwenye mchezo wa robo fainali ya kombe la shirikisho nchini, mchezo ambao utapigwa kwenye uwanja wa Namfua mjini Singida. 


Robo fainali hiyo imetokana na droo iliyochezeshwa leo na wachezaji wa zamani George Masatu aliyechezea Simba SC na Yahya Issa aliyechezea Yanga, chini ya usimamizi wa Ofisa wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jemedari Said.

Mechi hyo itakuwa ni marudio ya mechi ya kwanza ambapo timu hizo zilikutana kwenye uwanja huo wa Namfua kwenye raundi ya kwanza ya ligi kuu na kutoka sare ya 1-1.

Mbali na mchezo huo mechi nyingine za robo fainali zitakuwa kati ya Azam FC watakaokuwa wenyeji wa Mtibwa Sugar, Stand United watakaoikaribisha Njombe Mji FC na Tanzania Prisons watakaokuwa wenyeji wa JKT Tanzania.


Safari ya Yanga katika michuano hii ilianzia kwa kuiondoa Reha FC katika mechi ya hatua ya 64 kabla ya Yanga kusafiri hadi Mbeya na kuitoa Ihefu katika hatua ya 32 Bora kisha ikasafiri kwenda Songea katika hatua ya 16 Bora na kuitoa Majimaji na sasa itasafiri tena kwenda Singida.

Mechi za Robo Fainali zitachezwa kati ya Machi 30 na Aprili 1, mwaka huu katika viwanja vya Namfua, Singida, Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam, Sokoine mjini Mbeya na CCM Kambarage, Shinyanga.



No comments