KIWANGO CHA FEDHA KILICHOTUMIKA KWA USAJILI WA WACHEZAJI WOTE WA SIMBA MSIMU HUU NI SAWA NA THAMANI YA MCHEZAJI HUYU WA AL MASRY.


UNAWEZA kuhisi Al Masry walikosea kumuanzisha, Ahmed Gomaa na kumuweka nje Aristide Bance kwenye mechi yao ya juzi Jumatano dhidi ya Simba, lakini usichokijua ni kwamba straika huyo thamani yake inazidi kiwango cha fedha ambacho kilitumika kwa usajili wa wachezaji wote wa Simba msimu huu.


Kwa mujibu wa mtandao wa Transfermarkt.com, bei ya Gomaa mwenye umri wa miaka 29 sokoni kwa sasa ni Euro 600,000 (Sh1.7 bilioni) ambazo zingeweza kusajili kikosi chote cha Simba na chenji ikabaki. Kiasi cha fedha ambacho Simba imekitumia msimu huu kwa ajili ya kusuka kikosi chake kinachoongoza Ligi Kuu Bara kinakadiriwa kufikia Sh1.3 bilioni.

Hii inamaanisha kwamba kama Al Masry watamuuza Gomaa leo hii, mkwanja watakaovuta wanaweza kusajili kikosi chote cha Simba kilichocheza dhidi yao hiyo juzi. Kama hujamfahamu bado, Gomaa ni yule aliyevalia jezi namba 15 na ndiye aliyefunga bao la kusawazisha la Masry katika dakika ya 11.

Kwa mujibu wa taarifa za mtandao huo, kiwango hicho cha fedha ambacho kinatajwa kama thamani ya Gomaa sokoni kwa sasa, kinamfanya awe mchezaji ghali zaidi kwenye kikosi cha Al Masry akifuatiwa na beki raia wa Ivory Coast, Mohammed Koffi huku Mohammed Hamdi, Ahmed Shokry, Ahmed Ayman na Farid Shawky wakifuatia.

Koffi anayecheza beki wa kati, thamani yake ni Euro 500,000 (Sh1.4 bilioni), Hamdi na Shokry kila mmoja akiwa na thamani ya Euro 400,000 (Sh1.1 bilioni) wakati Shawky na Ayman wakiwa na thamani ya Euro 300,000 (Sh837 milioni).

 Katika hali ya kushangaza, mshambuliaji Aristides Bance ambaye ujio wake na kikosi hicho ulikuwa gumzo, hayupo hata katika orodha ya wachezaji watano wanaoongoza kwa thamani kubwa kwenye kikosi cha Al Masry.

Thamani ya Bance kwenye kikosi hicho kwa sasa ni Euro 200,000 (Sh558 milioni) fedha ambazo zinaweza kulipa mishahara ya Simba kwa miezi minne.

Follow us on Instagram @Tiktaktz ili uwe wa kwanza kupata taarifa mpya za michezo yote ndani ya nchi na nje ya nchi.

No comments