OKWI AJITABIRIA IDADI YA MAGOLI ATAKAYOWAFUNGA WAARABU UGENINI NCHINI MISRI.
STRAIKA wa Simba, Emmanuel Okwi, amewatuliza mabosi na
mashabiki wa timu hiyo akiwaambia wasiwe na presha ya marudiano na Al Masry
kwani anakwenda kupiga mabao ya kutosha. Amechimba mkwara kuwa anazifahamu
mbinu zote za mabeki wa Al Masry hivyo, ni lazima atawafunga tu kwao.
Simba ililazimishwa sare ya mabao 2-2 na Al Masry juzi
Jumatano usiku katika Kombe la Shirikisho, lakini staa huyo amesema nafasi yao
kusonga mbele bado ni kubwa.
Okwi, aliyeifungia Simba mabao 19 katika mashindano yote hadi
sasa msimu huu, alisema beki ya Al Masry inapitika na kwenye mchezo wa
marudiano atakuwa fiti zaidi hivyo, hawataweza kumzuia. Mganda huyo alisema
anajua watakapokuwa kwao watafunguka zaidi na hapo ndipo atakapowamaliza
kiulaini.
Nyota huyo aliyewahi pia kuzichezea Yanga, Etoile ya Tunisia
na Sondersjske ya Sweden, alisema kwa sasa wanapambana kwa ajili ya mechi ya
Ligi Kuu Bara, lakini tayari akili ameshaiweka sawa katika mchezo wa marudiano.
“Walikuwa wengi katika ukuta wao (juzi) tulipambana
kuwafungua na kufanikiwa kwa kiasi hicho, lakini sasa nimewajua vyema mabeki
wao,” alisema Okwi. “Kule kwao najua watafunguka na hicho ndiyo ninachokitaka,
nitawafunga wala sina wasiwasi.
Najua makocha wameona udhaifu wao na ubora wao, wala Wana
Simba wasiwe na shaka.” MIKAKATI KIBAO Kutokana na uzito wa mchezo wa
marudiano, viongozi wa Simba wameanza kuandaa mikakati ya ndani na nje ya
uwanja ili kwenda kuwang’oa Waarabu hao kwenye ardhi yao.
Kaimu Rais wa Simba, Salim Abdallah ‘Try Again’ amesema
wamejifunza kuhusu figisu za nje ya uwanja, hivyo hakuna wanalolihofia. “Simba
tumeamka na tupo tayari kupambana na figisu zote za nje ya uwanja huko, miaka
ya nyuma ndio walikuwa wanatuvuruga sio sasa,” alisema “Tutaifunga Al Masry
kwao, kama viongozi tayari tulishaanza kuandaa mikakati ya ndani na nje.”
LECHANTRE NAYE Kocha Pierre Lechantre alisema kama kuna siku
vijana wake walimfurahisha basi ni katika mchezo wa juzi na sasa anataka
kutulia na kufanya mambo mawili yatakayowapa matokeo mazuri ugenini. Alisema
mchezo wa ugenini utakuwa na sura tofauti ya ugumu hivyo, wanahitaji muda
mwingi wa kujiandaa.
Mfaransa huyo alisema anaiheshimu Al Masry, lakini endapo
watafanya maandalizi ya kutosha basi ana nafasi ya kuwang’oa Waarabu hao.
“Vijana wamenifurahisha, nafikiri kwa mara ya kwanza wamefanya kile
ninachokitaka kiwe katika timu ninayoifundisha, hatutakiwi kukata tamaa,”
alisema Lechantre.
Follow us on Instagram @Tiktaktz ili uwe wa kwanza kupata taarifa mpya za michezo yote ndani ya nchi na nje ya nchi.
Follow us on Instagram @Tiktaktz ili uwe wa kwanza kupata taarifa mpya za michezo yote ndani ya nchi na nje ya nchi.
Post a Comment